Ushiriki wa Watoto katika Vita dhidi ya Utumwa na Harakati za Kupinga Ukoloni nchini Tanzania: Uchunguzi wa Kazi Teule za Fasihi ya Kiswahili ya Watoto

Authors

  • Leonard H. Bakize University of Dar es Salaam

Abstract

Makala hii inachunguza ushiriki wa watoto katika vita dhidi ya utumwa na ujio wa wakoloni nchini Tanzania kupitia uchambuzi wa kazi teule za fasihi ya watoto na mwitiko wa wasomaji wa matini hizo. Tofauti na mtazamo wa kijamii unaowaona watoto kama kundi lisilo na sauti katika masuala mazito ya kihistoria, makala hii inathibitisha kwamba watoto walihusika moja kwa moja katika matukio hayo, ama kama wahanga na washiriki au kama wahifadhi wa kumbukumbu za kijamii. Makala hii imetumia mbinu mbili kuu: usomaji makini wa matini na majadiliano ya vikundi vya watoto wa shule za msingi (darasa la 5, 6 na 7) katika maeneo ya Dar es Salaam, Bagamoyo, na Morogoro Mjini. Uchambuzi umeongozwa na Nadharia ya Mwitiko wa Msomaji na Nadharia ya Jumuiya Zilizobuniwa. Nadharia ya kwanza imetumika kueleza namna watoto wanavyotengeneza maana wanaposoma matini za kihistoria, huku ya pili ikifafanua jinsi fasihi inavyounda hisia za utaifa, umoja, na utambulisho wa pamoja. Makala inaonesha kuwa fasihi ya watoto, hasa bunilizi za kihistoria, si chombo cha burudani tu bali pia ni nyenzo ya kijamii na kielimu inayowezesha watoto kushiriki katika ujenzi wa historia, kukuza fikra za ukombozi na kuimarisha utambulisho wa kitaifa. Kupitia usomaji wa matini na mijadala ya vikundi, watoto walionesha uwezo wa kufasiri upya masimulizi ya kihistoria kwa kuhusisha maadili ya utu, haki na usawa, wakijitokeza pia kama sehemu ya watengeneza historia. Kwa kutumia mitazamo ya nadharia hizi mbili, makala inathibitisha kuwa sauti za watoto zina mchango muhimu katika ujenzi wa kumbukumbu na uelewa wa pamoja wa jamii, hivyo, zinapaswa kupewa nafasi stahiki katika tafiti za kifasihi na kihistoria kuhusu Tanzania na Afrika kwa ujumla.

DOI: https://dx.doi.org/10.4314/kcl.v23i2.10

☍ View Article Analytics

Downloads

Published

2026-03-20